Thursday, May 20, 2010

Tanzania yapata tuzo ya Utalii huko Bondeni

Bodi ya Utalii Tanzania TTB hivi majuzi imeonyesha kwa waandishi wa habari TUZO waliyopata siku za hivi karibuni wakati wa maonyesho ya Utalii yaliofanyika mjini Durban, nchini Afrika Kusini kuanzia tarehe 8 hadi 11 Mei 2010. Maonyesho haya yanajulikana “INDABA, Travel Show” na yanafanyika kila mwaka nchini Afrika Kusini.

Maonyesho ya INDABA ni kati ya maonesho makubwa matatu ya utalii duniani, maonyesho mengine ni World Travel Market (WTM) yanayofanyika nchini Uingereza na ITB yanayofanyika nchini Ujerumani. Kwa miaka miwili mfululizo Maonyesho yameelezwa kama ndio maonyesho bora barani Africa

Tanzania ilishiriki kikamilifu kwenye maonyesho haya na Taasisi za Serikali nne ziliweza kushiriki ambazo Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Hifadhi za Taifa TANAPA, Mamlaka ya Bonde la Ngorongoro (NCAA) na Kamisheni ya Utalii Zanzibar.(ZCT)

Pamoja na taasisi za serikali, pia kulikuwa na kampuni binafsi 52 ambazo kati ya hizo 22 zilikuwa ni za kuongoza watalii (Tour Operators), 27 kutoka sekta ya hoteli, na kampuni 3 za ndege ziliweza kuwakilishwa.

Kama yalivyokuwa mashindano mengine, Tuzo hii linatolewa kila mwaka na nchi zote za 14 za SADC zinazoshindanishwa. Kwa mwaka huu TANZANIA ndio iliyoibuka kidedea na kutapa Tuzo ya kwanza “Platinum Award” na kuwashinda nchi zote nyingine za SADC pamoja na nchi ya jirani (Kenya). Kigezo kilichoshindanishwa ni pamoja na ubora wa banda, ushiriki wa sekta binafsi kwa maana bidhaa zilizokuwa zinauzwa, pamoja kauli mbiu yetu tuliyotumia mwaka huu ambayo ni “Experience the Real Game in Africa na nyingine “Celebrate FIFA world cup in Tanzania” WELCOME TO TANZANIA”, (“Karibu Afrika kwa Kombe la Dunia, Tembelea Tanzania Ujionee Vivutio vya Utalii”).

Bodi ya Utalii inajivunia Tuzo hii na inaahidi kuendelea kuongeza nguvu ya kutangaza, kuimarisha na kuboresha sehemu mbalimbali za vivutio vya utalii ikiwa ni pamoja na kudumisha ushirikiano wa kikazi na nchi za SADC, vile vile kuweza kutumia ujio wa Kombe la Dunia na FIFA nchini Afrika Kusini, kuvutia watalii wengi zaidi kuja kutembelea vivutio vya utalii nchini.

Wizara ya Maliasili na Utalii ikishirikiana na Bodi ya Utalii tumeweze kuwaleta waongoza utalii (Tour Operators) 38 kutoka Afrika Kusini kuja kutembelea vivutio vyetu ili waweze kuviuza kwa watalii wakati wa mashindano ya Kombe la Dunia. Vile vile, tumeweze kujitangaza kwenye majarida mbalimbali mashuhuri ya Afrika Kusini, na tunatarajia kushiriki tena maonesho mengine ya utalii yajulikanayo kama “World Tourism and Sports Destination Expo” yatakayofanyika tarehe 5 – 9 Juni 2010 kabla ya kuanza mashindano ya Kombe la Dunia.

Bodi ya Utalii inapenda kutoa shukrani kwa taasisi za serikali makampuni binafsi na wadau wote wa utalii waliofanikisha ushindi wetu na

Mwisho tunatoa shukurani kwa Wizara ya Maliasili na Utalii na Kamisheni ya Utalii za Zanzibar kwa ushirikiano mzuri waliotupa.

----------------------------------

Timu ya Tembea Tanzania inapenda kuchukua fursa hii kuipongeza TTB sambamba na wale wote walioiwezesha Tanzania kuibuka kidedea ktk mchakato huu. Mungu Ibariki Afrika, Mungu Ibariki Tanzania.

No comments:

Post a Comment