Thursday, October 27, 2011

Mto Rufiji Oktoba 2009 na Jinsi ulivyo sasa - Oktoba 2011

Picha hii niliipiga Oktoba 2009 nikiwa kwenye boti ndani ya Mto Rufiji. Ni moja ya picha ambazo nimekuwa nazo kwa kipindi kirefu kama taswira ya mto Rufiji. Hali hii imebadilika ghafla baada ya kukutana na hali tofauti nilipokwenda Selous/Mloka hivi karibuni. Picha hii ilikuwa ni nje ya Hifadhi ya Selous - usawa wa kijiji cha Mloka.

Oktoba 2009: Huu ni muonekano wa eneo la mbele la camp ya Hippo likionekana kuwa na maji ya kutosha kiasi cha boti zinazotumiwa na wageni kwa ajili ya boat rides kuweza kufika mpaka kwenye gati pembezoni mwa campsite. Hali ilivyo sasa ni tofauti na nilivyoiona mwaka 2009, japo mwezi ulikuwa ni huo huo - Oktoba.

Oktoba 2011: Hii picha nimeipiga nikiwa nimesimama mbele ya Hippo campsite, pembezoni kabisa na kingo za mto Rufiji (Ukiangalia picha ya kwanza, sehemu niliyosimama wakati nikipiga picha hii ni mbele ya hilo banda katikati ya hizo palm trees). Hii ilikuwa ni taswira ya kwanza kabisa kuipiga baada ya kuwasili campsite baada ya safari toka Dar. Ilinisononesha na kufuta kabisa taswira niliyokuwa nayo awali - ya kwanza, Oct 2009. Kauli ya mhudumu mmoja wa campsite "Bro!, mto Rufiji unakauka.." ilinimaliza kabisa.
Eneo ambalo linaonekana kuwa na kisiwa cha mchanga ni eneo ambalo mwaka 2009 niliipiga picha Hippo campsite tokea kwenye Boti. sasa hivi naweza kufika hapo kwa kutembea bila hata ya kuhitaji Boti [Angalizo kwa usiye mwenyeji, usijaribu kuvuka kwa miguu bila ya kuwa na wenyeji wa kukuongoza]

Oktoba 2011: hapo ndipo maboti yalikuwa yanaegeshwa na kupakia abiria wanaofanya boat safari kwenye mto Rufiji. Sasa hivi hakuna hata boti moja. Imebidi zihamishiwe eneo jingine kutoka na kina cha eneo hili kupungua na kufanya boti kushindwa kuelea kabisa. Sasa hivi boat safaris zinaanzia kwenye maeneo machache ambayo ndio yana kina kirefu kando kando ya mto Rufiji. Kila upande utakaoangali utaona ni robo tu ya eneo ndilo lina maji. Robo tatu likiwa limegeuka kuwa kisiwa cha mchanga.

Oktoba 2011: Wenyeji wangu walinieleza ya kwamba siku hizi vijana huenda kufanya tizi kwenye visiwa hivi vya mchanga. Wenye campsites nao wamekuwa wabunifu kwa kuwatengea chakula cha jioni wageni kwenye visiwa hivi na kuwapa candle light dinner ya ukweli.

Viboko ambao mwaka 2009 walikuwa makundi mengi huku kila kundi likiwa na viboko wasiopungua sita, kwa hivi sasa ni kama wametoweka kabisa. wengi wamekimbia kabisa eneo hili kutokana na kupungua kwa kina cha maji na kwenda maeneo mbalimbali ambayo wanajiona wapo salama. Ukiwahi kuamka asubuhi unaona alama za miguu ya viboko walipopita usiku wakiwa safarini kutoka majini kuelekea nchi kavu kutafuta chakula - majani. Kimsingi hali ya kina cha maji ya mto Rufiji ni mbaya na nikiutumia mto huu kama kielelezo, basi tuna hali mbaya au tunelekea kubaya.
Nilibahatika kumuuliza mdau mmoja wa mazingira kuhusu hali hii na yeye akasema haya ni matokea ya kutosimamia vyema matumizi ya maji ya mito na kulinda vyanzo vya mito hii. Sambamba na uharibifu wa mazingira ktk vyanzo vya mito hii. Mto Ruaha ni moja ya mito inayomwaga maji yake ktk mto Rufiji. Nilitonywa kuwa Mto Ruaha nao haupo poa sasa hivi.

No comments:

Post a Comment